Saturday, August 18, 2012

Namna ya kupanga malengo maishani


                                                                                        
Baada ya kuanza kujiuliza na kuyatambua malengo yako huku ukiandika kila wazo linalokujia akilini, fuata hatua zifuatazo:

1. JENGA PICHA AKILINI MWAKO
Jenga taswira ya kitu unachokitaka akilini mwako. Picha unayoijenga lazima iwe kubwa. Fikiria jinsi utakavyokuwa na mafanikio makubwa maishani katika kile ulichochagua kukifanya. Jione tayari ukiwa katika mafanikio ambayo ulikuwa ukiyatamani kwa siku nyingi.

Jitazame furaha utakayokuwa nayo na jinsi utakavyoyamudu maisha ya mafanikio. Panga malengo ya muda mrefu. Usifikirie kuwa ulichokiwaza kitatokea kesho, jipe muda hata wa miaka kumi au zaidi, usiogope kufikiria mambo makubwa yanayohitaji muda mrefu kukamilika. Kuanzia hapo, endelea na hatua ya pili.

2. YARAHISISHE MALENGO YAKO
Yawezekana malengo yako ni makubwa sana kiasi cha kukuzidi. Hiyo isikutishe, yarahisishe malengo yako. Kivipi? Kama malengo yako ni kuwa na mafanikio makubwa maishani baada ya miaka kumi, ugawanye muda wako katika sehemu ndogondogo.

Kwa mfano unaweza kuanza kugawanya miaka kumi kwa mbili, yaani baada ya miaka mitano uwe angalau umefikia nusu ya kile ulichokiwaza awali. Baada ya hapo igawanye miaka mitano kupata mwaka mmoja mmoja.

Jiulize kwa kila mwaka utafanya nini ili kuyakaribia mafanikio. Weka ratiba na mipango yako kwa maandishi. Ugawanye mwaka kupata miezi, jiulize utafanya nini mwezi wa kwanza, wa pili hadi mwaka uishe. Hakikisha unaandika kila kinachokujia akilini.

Endelea kurahisisha malengo yako kwa kujiuliza ndani ya miezi sita utakuwa tayari umefanya nini, shuka mpaka miezi mitatu kisha malizia kwa kila mwezi mmoja. Utaona kwamba lengo unalotarajia kulifanikisha kwa kipindi cha miaka kumi umelirahisisha mpaka kwenye mwezi mmoja.

Usiishie hapo, mwezi ugawanye kwenye wiki, kisha malizia kwenye siku. Jiulize kila siku utafanya nini ili kuelekea kwenye lengo lako kubwa unalotaka litimie baada ya miaka kumi. Hapo utaanza kuona umuhimu wa kutumia muda wako vizuri, hakuna muda wa kupoteza.

3. ANZA UTEKELEZAJI
Anza utekelezaji wa malengo yako mara moja. Hakikisha kila saa inayopita umefanya jambo ili kupalilia malengo yako. Hakikisha unafuata ratiba uliyojipangia, usisubiri mtu mwingine aje kukukumbusha kuhusu malengo uliyoyapanga. Tembea na karatasi au kitabu ulichoandika malengo yako na endelea kujikumbusha kila siku juu ya kile unachotaka kitokee.

Mwanasaikolojia mmoja mashuhuri aliwahi kuandika kuwa: Mafanikio siyo tukio unaloweza kulisubiri litokee bali ni hatua unayochukua kuyafikia. Ukianza kufikiria mafanikio, tayari umeanza kufanikiwa, ukiweza kupanga malengo na kuanza kuyafanyia kazi, tayari umo ndani ya mafanikio.

Usisubiri itokee siku ambayo utalala halafu ukiamka asubuhi ukute yale uliyokuwa unayataka yametokea. Malengo yako lazima yakutese usiku na mchana. Watu wote waliofanikiwa hawakufika hapo kwa bahati, walipanga malengo na wakayafanyia kazi.

MAMBO YA KUZINGATIA KUELEKEA MAFANIKIO
Kwa kuwa maisha ni kama safari na malengo ndiyo dira, ukianza kuyafanyia kazi malengo yako utagundua unatakiwa kufanya nini ili safari yako ya maisha iwe rahisi. Lazima ufahamu mambo muhimu yatakayokusaidia kurahisisha safari yako kuelekea mafanikio.

Labels: ,

0 Comments:

Post a Comment

Subscribe to Post Comments [Atom]

<< Home