Saturday, August 4, 2012

MAMBO 10 YANAYOMFANYA MWANAUME AKOSE UAMINIFU..


Kutokuaminiana baina ya watu/ wapenzi siku hizi imekuwa ni kitu cha kawaida sana, vyombo vingi vya habari ikiwemo radio, television na mitandao ya kijamii vimekuwa vikiripoti sana matukio ya wapenzi kutokuwa waaminifu. Kwa leo sasa nataka kuzungumzia KWANINI WANAUME WANAKOSA UAMINIFU.

Wanaume  wote wanajua kwa kiasi kikubwa kuwa “udanganyifu” kwenye mapenzi si kitu kizuri wala si sahihi. Japo hata katika maandiko matakatifu tunaambiwa “USIZINI” tena wengi wetu wanasema kuibanjua “amri ya sita” na kweli bado wanabanjuka.
Kwenye mahusiano yasiyo imara au yenye mvurugiko, mara nyingi udanganyifu huwa ni suluhisho la muda mfupi la mwanaume, kwani huwa anafikiri kwa kuwa na mwanamke nje basi atakuwa amemaliza mvurugano wa ndani ya nyumba yake.

Hivi karibuni nimekuwa naongea na kudadisi wanaume ni nini kinawafanya wanakuwa wadanganyifu na zifuatazo ni sababu zao walizotoa.

1.      Mke kutojiachia kwenye mapenzi
Wanaume wengi wanalalamika kuwa wake zao hawajiachii wanapokuwa faragha. Unakuta mwanamke hataki kuonekana kama “kahaba” kwa mumewe hivyo kujikuta wana aina ya kufurahia lile tendo kwa ustaarabu na heshima nyingi na inakuwa kila siku ni hivyo hivyo. Wakati mwanaume anataka kila mara wajaribishe kitu kipya.
2.      Kufuata Mkumbo
Baadhi ya wanaume wanasema wanafanya hivyo ili kufanana na rafiki zao au watu wao wa karibu, kuna mwanaume anathubutu kusema amerithi kwa “babu” yake kwani naye alikuwa anapenda sana wanawake. Mwanaume mwingine anasema yeye rafiki zake wote wanapokuwa sehemu za starehe huwa na wanawake tofauti na wake zao hivyo na yeye inabidi kuwa na mwanamke ili kufanana na company yake kwani akistick kwa mkewe rafiki zake watamtenga.

3.      Kujiongezea Umaarufu/ (Kidume cha Mbegu)
Wanaume kuna wakati wanakuwa wanajaribu kuangalia soko lao likoje, unakuta mwanaume anaanza kuhofia kuwa umaarufu wake kwa wanawake unapungua hivyo anaanza kutongoza kila mwanamke aone anakubalika kiasi gani. Matokeo yake anapata wanawake kadhaa na kujikuta yupo mtegoni na tayari amejitumbukiza kwenye nyumba ndogo.

4.      Upenyo Kidogo Tu
Inawezekana mwanaume hakuwa na lengo la kuwa na mwanamke tofauti na mkewe, lakini unakuta huyu mwanaume labda ameenda bar au sehemu yoyote ya starehe na kukuta mwanamke amevalia mavazi yanayohamasisha ngono basi hapo mwanaume akijaribu kumpata huyu mwanamke na akafanikiwa ndio imetoka hiyo – “nyumba ndogo”.
5.      Karaha za Mke
Wanawake mara nyingine huwa ni sababu kubwa ya mwanaume kutafuta nyumba ndogo. Unakuta mwanamke ana mdomo, mumewe akifika tu nyumbani ugomvi umeanza, karaha moja kwa moja. Mume anatafuta suluhisho kwa kuondoka nyumbani kwenda kupumzika sehemu ili kupunguza karaha, kule anakoenda anakutana na mwanamke ambaye mara nyingi huwa wana mitego sana (kwa kuwa wanajua mwanaume akiwa bar peke yake basi anakuwa anakimbia maudhi ya mkewe)
6.      Wanawake wanawalegezea
Kiukweli wanawake wana huruma sana na ni wepesi wa kusamehe hasa kwa tabia mbaya za waume zao. Inawezekana na kwa kuwa na hofu ya kuishi peke yao au kwa kuwa huwa hawapendi kukuza mambo. Kuna wakati mwingine wanawake wengine huwa wanaweza hata kujilaumu wenyewe kwa waume zao kutokuwa waaminifu kwenye mahusiano na wao (wanawake) kuchukua hatua za ziada ili kuimarisha huo uhusiano kama huamini muulize Bill Clinton.

7.      Kazi na Maumbile
Maumbile ya wanaume mara nyingi hayawezi kuvumilia kwa muda mrefu bila kushiriki lile tendo, sasa iwapo mwanaume atakuwa na kazi ambayo itamlazimu kusafiri au kuwa mbali na familia ni dhahiri atajikuta keshavunja uaminifu.

8.      Uhuru Uliopitiliza/ Kutelekezwa
Mwanaume anaondoka asubuhi na kurudi usiku mwingi lakini mkewe wala hamuulizi alipotoka wala hata kujua mwenendo wake kwa ujumla, matokeo yake mwanaume anakuwa na muda mwingi na akishawishiwa na wanawake wa mabarabarani basi kwa kuwa muda upon a hakuna anayemuuliza ulikuwa wapi au utarudi saa ngapi basi anatumia uhuru wake kwa mambo yasiyo na manufaa.

9.      Ushawishi wa Wanawake
Dunia imeharibika na kuna wanawake wamejaa na kwa ubovu wa tabia zao unakuta hawajapata kuolewa hivyo wanabuni mbinu za kuchukua waume wa wenzao. Unakuta mwanamke anajua kabisa kuwa huyu ni mume wa mtu lakini atamganda hadi ajigandishe kwa huyo mwanaume. Katika hali ya kawaida mwanaume kushinda vishawishi au uchochezi wa mwanamke anayemtaka inakuwa ngumu, kwanza utaonekana si mzima maana mwanamke anajileta halafu umkatae, kila mwanaume (asiye na akili) atakushangaa.
10.  Kutokuwa na hofu ya Mungu
Ukiwa na hofu ya Mungu kamwe huwezi kufanya yasiyompendeza Mungu, wanaume wengi huwa hawana hofu ya Mungu na hiyo ndiyo sababu kubwa inayowafanya kuwa na uthubutu wa kufanya hayo kwa ujasiri na visingizio vingi.

HITIMISHO: Ewe mwanaume kama utaona huna mapenzi tena na mkeo wala hamuwezi kukaa na kujadili matatizo yenu ni bora kuwa muwazi ili kuangalia suluhisho kuliko kuwa na “mahawara”  Kumbuka kuwa udanganyifu si kitu chema mbele za Mungu. Kama si mwaminifu kwa mkeo ina maana humo ndani kwenu hakuna amani au kuna matatizo ambayo hamjayazungumza. Iangalie hiyo hali ya wewe kukosa uaminifu kwa jicho la tatu na utaona kuwa kukosa uaminifu ni tatizo kubwa zaidi kuliko hayo madogo ambayo yapo kati yenu na hamyazungumzii. Udanganyifu utakufanya ujisikie vizuri kwa muda lakini hakuna suluhu ya aina hiyo kwani tatizo la ndani mtakuwa hamjalimaliza hata kidogo.

Labels: ,

0 Comments:

Post a Comment

Subscribe to Post Comments [Atom]

<< Home