Tuesday, August 21, 2012

DR KAFUMU (CCM) AVULIWA UBUNGE NA MAHAKAMA IGUNGA




MAHAKAMA KUU ya Kanda ya Tabora leo imemvua rasmi ubunge, Dk Peter Kafumu, aliyekuwa Mbunge wa Igunga kupitia Tiketi ya CCM katika uchaguzi mdogo uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana.

Hukumu hiyo imetolewa baada ya mlalamikaji Joseph Kashindye aliyekuwa mgombea ubunge kupitia Tiketi ya Chadema kufungua kesi dhidi ya Peter Kafumu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo.
Katika shauri hilo, hoja 15  ziliwasilishwa na wakili wa upande wa mlalamikaji Profesa  Abdalla Safari ikiwamo anayodai kwamba Waziri wa Ujenzi  John Magufuli alifanya mkutano wa kampeni Kata ya Igulubi wilayani Igunga kutumia madaraka yake kuahidi ujenzi wa Daraja la Mbutu kama wananchi hao watampigia kura mgombea wa chama mapinduzi.

Pia Safari anadai waziri huyo aliwatisha wananchi wa kata hiyo kwamba wasipo ichagua CCM daraja hilo halitajengwa na kwamba pia aliwatisha wananchi hao kuwa wasipomchagua Dk Kafumu watashughulikiwa.
Profesa Safari alidai  Baraza la Waislamu (Bakwata) Wilaya ya Igunga liliwakataza waumini wasiipigie kura Chadema  na kwamba naye Rais mstaafu, Benjamini Mkapa alitoa ahadi ya kugawa mahindi kwa wananchi wa Igunga siku moja kabla uchaguzi ili waichague CCM.

Labels: ,

Friday, August 17, 2012

Rufaa Ya Lema Tarehe 20 Sept



RUFAA ya kupinga kuvuliwa ubunge ya aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema (CHADEMA), imepangwa kusikilizwa Septemba 20, mwaka huu, mbele ya majaji watatu wa Mahakama ya Rufaa; Natalia Kimaro, Mbarouk Salim Mbarouk na Salumu Massati.
Kwa mujibu taarifa za kikao cha Mahakama ya Rufaa cha Arusha, rufaa hiyo iliyofunguliwa na Lema akipinga uamuzi uliotengua ubunge wake kufuatia shauri lililofunguliwa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, inatarajiwa kusikilizwa kwa siku moja ambapo baada ya hapo itapangwa tarehe kwa ajili ya kutoa uamuzi.

Awali, Lema kupitia wakili wake, Method Kimomogoro, aliwasilisha kwenye mahakama hiyo hoja 18 za madai akipinga kutenguliwa kwa ubunge wake na Mahakama Kuu Kanda ya Arusha Aprili 5, mwaka huu.

Kwenye baadhi ya madai hayo, Lema aliiomba Mahakama ya Rufaa kutengua uamuzi wa Mahakama Kuu, uliotengua ubunge wake, huku akiitaka imtangaze kuwa mbunge halali wa Jimbo la Arusha Mjini.

Aidha, aliitaka mahakama hiyo ya juu, iwaamuru walalamikiwa katika shauri hilo walipe gharama za rufaa hiyo pamoja na zile za kesi iliyomalizika kwenye Mahakama Kuu Kanda ya Arusha.

Katika madai mengine, Lema anamlalamikia, Jaji Gabriel Rwakibarila, aliyesikiliza kesi hiyo kuwa, alitoa uamuzi wake kwa kuzingatia maneno ya uvumi, huku akipuuza ushahidi uliotolewa mahakamani hapo.

Lema anadai kuwa, Jaji alikosea wakati alipoamua kuwa mpiga kura yeyote anaruhusiwa kupinga matokeo ya uchaguzi hata kama haki zake za msingi hazijaguswa.

Kesi hiyo iliyotengua ubunge wa Lema, ilifunguliwa na wanachama watatu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM); Mussa Mkanga, Agness Mollel na Happy Kivuyo, wakidai kuwa wakati wa kampeni mbunge huyo alimdhalilisha mgombea mwezake, Dk. Batilda Burian kwa kutumia lugha za matusi.

ANGALIZO
Jaji Mbarouk Salim Mbarouk ni yule aliyeonekana kutajwa kwa namna isiyo nzuri kwenye utetezi wa Tundu Lisu au ni mwingine? na kama ni yeye hiyo haitaleta tena kutoridhika iwapo maamuzi hayatakuwa upande wa Lema na Chadema? nini mawazo yenu katika hili? 
Bush Lawayer

Labels: ,

Sunday, August 12, 2012

MNYIKA : CCM WANA UZUSHI WA KIJINGA KUWA CHADEMA IMEPEWA MABILIONI NA NCHI ZA NJE..


                                                            Mh. John Mnyika, mbunge wa Ubungo.                                                                          

Kauli ya awali kufuatia madai ya kizushi na kijinga ya CCM kuwa CHADEMA imepewa mabilioni na nchi za nje

Katika mitandao ya kijamii kumesambazwa habari zikimnukuu msemaji wa CCM kutoa madai mbalimbali ya uzushi katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu CHADEMA baada ya CHADEMA kuendelea kutekeleza mikakati na mipango yake ya kuwaunganisha watanzania kupitia falsafa ya ‘nguvu ya umma’ katika kuchangia vuguvugu la mabadiliko (M4C) katika maeneo mbalimbali nchini. Nitatoa tamko kamili na kueleza hatua za ziada baada ya kupata taarifa iliyotolewa kwa ukamilifu, hata hivyo kuhusu madai yaliyokwisha sambazwa kwenye mitandao ya kijamii na CCM nachukua fursa hii kutoa kauli ya awali kama ifuatavyo:


Kuibuka huku kwa CCM na kufanya propaganda chafu ni ishara ya kwamba CCM inaumizwa na namna ambavyo watanzania wanajitokeza kuunga mkono CHADEMA kwa hali na mali hivyo CCM sasa inatapatapa kujaribu kudhibiti wimbi la mabadiliko kwa kutumia siasa chafu. Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya Kikwete anapaswa kueleza watanzania iwapo mikakati hiyo michafu ina baraka zake na za serikali anayoiongoza kwa kurejea pia madai yaliyotolewa na Waziri wa Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu) Steven Wassira kuwa CHADEMA itasambaratishwa katika kipindi cha mwaka mmoja kwa mbinu mbalimbali.

CCM kwa kuwa imekuwa na kawaida ya kufanya usanii kuhalalisha fedha haramu kama ilivyofanya kwenye chaguzi zilizopita baada ya viongozi waandamizi wa CCM na makada wake kuchota fedha za chafu kifisadi kama zile za kutoka kwenye Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) na vyanzo vingine vichafu na kuzisafisha kupitia harambee za hadaa zilizofanywa na CCM kwa nyakati mbalimbali; inataka kuichafua CHADEMA inayopata fedha kutoka vyanzo halali kwa njia za wazi ili kukatisha tamaa umma wa watanzania unaochangia vuguvugu la mabadiliko.

Viongozi wa CCM wameamua kujidanganya, kuidanganya Serikali yao na kujaribu kuwapotosha watanzania lakini CHADEMA inatambua kwamba watu wachache wanaweza kudanganyika kwa muda mchache lakini si watu wote wakati wote; na kwamba watanzania wa leo kwa uwingi wao hawawezi kudanganyika na uzushi wa kijinga wa CCM.

Ni ukweli ulio wazi kwamba CHADEMA imekuwa ikifanya harambee kwa uwazi kwa nyakati mbalimbali katika kumbi na katika mikutano ya hadhara ikiwemo ya vijijini ambapo michango hutolewa kwa uwazi, aidha michango kwa njia ya simu inaweza kufuatiliwa na kuthibitisha bila shaka yoyote kwamba watanzania wameamua kuchangia mabadiliko ya kweli.

Madai ya CCM kuwa CHADEMA imepokea au itapokea mabilioni ya shilingi kutoka mataifa ya nje ni ya uzushi na narudia kwa mara nyingine tena kuitaka CCM itaje majina ya serikali, taasisi ama makampuni ya nje ambayo CCM inadai kwamba CHADEMA imepokea mabilioni ya shilingi katika siku za karibuni au inatarajia kupokea.

Badala ya CCM kuisingizia CHADEMA ilipaswa CCM ieleze watanzania orodha ya vigogo wa Serikali inayoongozwa na wanachama waandamizi wa CCM ambao wanaelezwa kuwa na akaunti nchini Uswisi na nchi zingine wakituhumiwa kupewa fedha za kifisadi kutoka kwa makampuni ya utafutaji wa mafuta, gesi asili pamoja na uchimbaji wa madini.

CCM ilipaswa ieleze watanzania sababu za kuendelea kusuasua kujivua magamba ya ufisadi kinyume na maazimio ya CCM yaliyofikiwa baada ya msukumo wa CHADEMA kutaja orodha ya mafisadi kwa kuwa kati ya mafisadi hao ni pamoja na viongozi wa CCM walioiingiza nchi katika mikataba mibovu.

Ikumbukwe kwamba madai haya si mapya kutolewa na CCM, yaliwahi kutolewa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) Sophia Simba mara baada ya uchaguzi mkuu wa 2010 akidai kuwa CHADEMA imepokea fedha kutoka mataifa ya ulaya kwa ajili ya kufanya maandamano ya kuiondoa CCM madarakani.

Itakumbukwa kwamba wakati huo nilimtaka ataje nchi hizo na kueleza kusudio la kumchukulia hatua zaidi na kwa upande mwingine niliyataka mataifa hayo ya Ulaya yatoe kauli kuhusu madai hayo. Izingatiwe kwamba mataifa hayo yalikanusha madai hayo ya CCM na Sophia Simba mwenyewe alikana kuwa hakuna madai hayo dhidi ya CHADEMA.

Nimeelezwa kuwa CCM imetoa madai mengine ya uzushi kuwa CHADEMA inapewa mabilioni toka nje kwa kuwa nchi imegundua rasilimali za mafuta na gesi na kudai kuwa fedha hizo ni kwa ajili ya kuiweka nchi rehani.

Madai haya yaliwahi kutolewa pia na Katibu wa CCM wa Fedha na Uchumi Mwigulu Nchemba na nikamtaka Waziri wa Mambo ya Nje Benard Membe kutaja nchi hizo na mikataba hiyo hata hivyo mpaka sasa hakuna kiongozi yoyote wa CCM na Serikali aliyejitokeza kutaja CHADEMA imepokea au itapokea mabilioni kutoka nchi gani na kwa mikataba gani.

CCM inatoa madai hayo kuhamisha mjadala baada ya CHADEMA wa uongozi bora, sera makini, mikakati sahihi na oganizesheni thabiti kuwa mstari wa mbele katika kutetea rasilimali za taifa na watanzania kutambua kwamba taifa letu litaepushwa kutumbukia kwenye laana ya rasilimali kwa kuiondoa CCM madarakani katika chaguzi za mwaka 2014 na 2015 na kuichagua CHADEMA.

CCM na Serikali yake ndiyo imekuwa kinara wa kupokea fedha kutoka nje kwa kisingizio cha misaada na kuingia mikataba mibovu na mataifa ya nje pamoja na makampuni ya kigeni na kuachia mianya ya uporaji wa rasilimali za nchi na CHADEMA imeanika hali hii kwenye orodha ya mafisadi kwa kutaja majina ya viongozi waliohusika kwenye mikataba ya madini na tutaendelea kufanya hivyo hata katika masuala ya mafuta na gesi ambayo tayari vigogo wa Serikali inayoongozwa na CCM wameshaanza kuingia mikataba mibovu na kuingiziwa fedha katika akaunti zao za nje ya nchi.

Hivyo, badala ya CCM kutoa madai ya uzushi kuhusu CHADEMA kuingia mikataba na serikali au makampuni ya nje, CCM ieleze watanzania imechukua hatua gani mpaka sasa juu ya viongozi na wanachama wake waliongia mikataba mibovu kwenye rasilimali muhimu nchini ikiwemo madini, mafuta, gesi na maliasili zingine za taifa letu na kutoa mikataba hiyo hadharani ili watanzania waweze kuchukua hatua za kufanya mabadiliko ya kweli.

Hivi karibuni Rais Kikwete ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM alisema kwamba serikali inayoongozwa na CCM haitarudia makosa ya kuachia mianya ya ufisadi kwenye gesi; hivyo CCM ilipaswa wakati huu kuwaomba radhi watanzania kwa ufisadi uliofanyika kwenye madini na rasilimali nyingine na kuishukuru CHADEMA kwa kuendelea kuwaunganisha watanzania wakati wote kusimamia mabadiliko ya kweli.

CCM badala ya kutishia kuwa ina mikataba inayoihusu CHADEMA ingetoa mikataba hiyo na hali hii ya CCM inayoongoza Serikali kudai CHADEMA kufanya mikakati, mipango na shughuli iliyo kinyume cha sheria bila vyombo vya dola kuchukua hatua ni ishara ya CCM kukiri wazi kuwa chama legelege chenye serikali legelege kimeshindwa kuongoza nchi na badala yake kimejikita katika propaganda chafu.

CHADEMA tangu kuanzishwa kwake imekuwa na makubaliano ya ushirikiano (MOU) bila masharti yoyote na vyama rafiki vya ndani ya Afrika na duniani na makubaliano hayo yamekuwa yakifikiwa kwa uwazi ikiwa ni sehemu ya CHADEMA kuwa na mtandao wa kimataifa na hayajawahi kuhusisha wala hayatawahi kuhusisha CHADEMA kusaidiwa mabilioni ya shilingi kwa ajili ya kufanya kazi zake kama inavyodaiwa na CCM.

CHADEMA kimekuwa chama kiongozi kwa nyakati mbalimbali kueleza viwango cha matumizi yake ya fedha na vyanzo vya fedha husika huku kikitegemea kwa kiwango kikubwa michango ya wanachama na wapenzi wa chama hapa nchini pamoja na kutumia kwa ufanisi ruzuku inayotolewa kwa vyama vya siasa.

CCM imekuwa na kawaida ya kutoa madai ya uzushi wakati mwingine yakiambatana na kutoa nyaraka za kughushi inazodai kuwa ni za CHADEMA. Ikumbukwe kwamba wakati wa uchaguzi wa mdogo wa Igunga, CCM ilitoa madai ya uzushi kuwa CHADEMA inafadhiliwa na nchi za nje ikiwemo kupewa mafunzo ya ugaidi na kudai kuwa tayari magaidi wameingizwa na CHADEMA toka nje katika uchaguzi huo; hata hivyo katika mwenendo wa kesi ya uchaguzi ya Igunga Katibu Mkuu wa CCM Wilson Mukama aliyetoa madai hayo alitoa ushahidi mahakamani kwamba CHADEMA haijawahi kuleta magaidi bali kauli hizo za CCM zilikuwa ni za siasa za uchaguzi.

Hivi karibuni, CCM imeghushi waraka mwingine na kuusambaza kile ilichodai kuwa ni maazimio ya kamati kuu ya CHADEMA ya kupanga migomo ya walimu, madaktari na mipango mingine ya kuhujumu serikali; hata hivyo waraka huo ulidhihirika wazi kuwa ni wa kughushi.

Mikakati yote hiyo michafu hupangwa na CCM mara kwa mara wakati ambapo CHADEMA inaanza operesheni Sangara na mikakati mingine ya kuleta mabadiliko nchini na kujipanga kuiondoa CCM madarakani kama ilivyo sasa ambapo CHADEMA inaendelea na operesheni katika mkoa wa Morogoro hivyo watanzania wanapaswa kuipuuza CCM na kuendelea kujiunga CHADEMA na kuchangia mabadiliko kwa hali na mali mpaka kieleweke.

John Mnyika (Mb)

Mkurugenzi wa Habari na Uenezi

source; mnyika.blogspot.com

Labels: ,

Rungu la Dk Mwakyembe latua kwa meneja Tazara

                                                                     

WAZIRI  wa Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe amesema atamtimua kazi Meneja Mkuu wa Shirika la Reli la Tanzania na Zambia (Tazara), Abdallah Shekimweri, iwapo atashindwa kusimamia majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuwapa vitendea kazi na posho wafanyakazi wa shirika hilo.
Rungu la waziri huyo lilianza Juni 5, mwaka huu baada ya kutengua uteuzi wa aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Paul Chizi na kumteua rubani wa muda mrefu, Kapteni Lusajo Lazaro kukaimu nafasi hiyo.
Mbali na uteuzi huo pia alitangaza kuwasimamisha kazi vigogo wengine wanne wa shirika hilo ambapo baada ya siku chache alianika ufisadi unaodaiwa kufanywa na kigogo huyo.
Lakini jana wakati akiwa katika ziara yake ya kushtukiza katika karakana za Tazara, Dk Mwakyembe alisema kuwa haridhishwi na utendaji kazi wa Shekimweri.
Mbali na kutembelea Tazara, pia alifanya ziara  bandarini na katika ofisi za Kampuni ya Reli Tanzania (TRL).
Akiwa katika ziara hiyo aliahidi kukutana na uongozi mzima wa Tazara ili kujadili matatizo yaliyopo katika shirika hilo ikiwa ni pamoja na ubovu wa reli, lengo likiwa ni kuyapatia ufumbuzi.
Mmoja wa wasaidizi wake ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini licha ya kuwa alikuwa amembatana na waziri huyo katika ziara hiyo alisema kuwa suala la kumtimua kazi Shekimweri siyo jambo la utani.
“Dk Mwakyembe ameshatuma barua kwa uongozi wa Tazara nchini Zambia, amewaeleza wazi kuwa haridhishwi na utendaji kazi wa (Shekimweri) na yupo tayari kutoa uamuzi, itakuwa kabla ya Oktoba mwaka huu,” alisema  msaidizi huyo na kuongeza;
“Si unajua hili shirika linaendeshwa kwa ubia wa Tanzania na Zambia, hivyo kama unataka kuchukua uamuzi ni lazima upande mwingine uwe na taarifa.”
Dk Mwakyembe alisema haridhishwi na ufanyaji kazi unavyoendelea katika Karakana ya Tazara na kumtaka Shekimweri kuwapa vifaa wafanyakazi hao na iwapo atashindwa kufanya hivyo atalazimika kumfukuza kazi. “Tutafukuzana hapa, watu wapo tayari kufanya kazi ila  wanakwamishwa, mwambieni Shekimweri kuwa nitamfukuza kazi na nitarudi tena Jumatatu (kesho),” alisema Dk Mwakyembe.
 Alisema kuwa ni jambo la ajabu kwa menejimenti ya Tazara kushindwa kutoa fedha kwa watumishi wake wakati Serikali imeshatoa fedha za ukarabati wa mabehewa ya treni yanayotakiwa kuanza kutoa huduma ya usafiri kuanzia Oktoba mwaka huu.
 Dk Mwakyembe alihoji sababu ya menejimenti hiyo kukalia fedha hizo wakati zinapaswa kulipwa kwa wafanyakazi hao wanaoendelea kukimbizana na muda ili kumaliza ukarabati huo. “Fedha mnaziweka makao makuu kwani ni maua hayo? Walipeni watu fedha zao na mnunue vifaa, tutafukuzana hapa na hakuna wa kunilaumu,” alisema Dk Mwakyembe.
Aliitaka menejimenti ya Tazara kukamilisha ukarabati wa mabehewa 14 ambayo aliagiza yafanyiwe ukarabati kwa kuwa mpaka sasa ni mabehewa manne tu ndiyo yanayoonekana kukarabatiwa.
Baadhi ya wafanyakazi waliokuwapo katika maeneo yao ya kazi walimweleza, Dk Mwakyembe kwamba shirika hilo haliwawekei fedha zao za mifuko ya hifadhi ya jamii, suala ambalo waziri huyo aliahidi kulifuatilia kwa ukaribu.
Akiwa katika Karakana ya TRL, Dk Mwakyembe aliridhishwa na utendaji kazi na kusema kuwa mpaka Oktoba mwaka huu treni ya Reli ya Kati itaanza kutoa huduma zake kama ilivyotangazwa.
Katika hatua nyingine, Dk Mwakyembe alisema mashine ya kushusha na kupakia mizigo katika meli karibu itafungwa kwa kuwa ujenzi wa reli kwa ajili ya kusimamisha mashine hiyo unaendelea vizuri.
source: Mwananchi, Jumapili.

Labels: ,

Friday, August 10, 2012

HATIMAYE MALAWI YASALIMU AMRI KWA TANZANIA..

Siku chache baada ya Serikali ya Tanzania kupitia kwa waziri wake wa mambo ya nje Mh. Bernad Membe kuitaka Serikali ya Malawi kuondoa majeshi na kampuni zinazofanya utafiti wa gesi kwenye ziwa Nyasa ukanda wa Tanzania wakidai kuwa ziwa hilo ni la kwao lote wameanza kufanya hivyo na kuondoka taratibu ukanda huo. Kwa mujibu wa mkuu wa mkoa wa Mbeya Bw. Abbas Kandoro alisema kuwa kwa sasa eneo hilo hali ni shwari kwani

makampuni, ndege na askari wa malawi waliokuwa wakiendesha shughuli zao kwenye eneo la Tanzania wametii amri na kuondoka kwenye eneo hilo hivyo wananchi wasiwe na shaka bali waendelee na kazi zao za kila siku kwenye ziwa hilo, Mbali na Waziri Membe, viongozi wengine waliozungumzia mgogoro huo na

kuitaka Malawi iache uchokozi ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika

Mashariki, Samuel Sitta na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya

Nje, Ulinzi na Usalama, Edward Lowassa.

Labels: ,

Wednesday, August 8, 2012

NAIBU WAZIRI ABUDULLAH JUMA APATA AJALI MBAYA


Naibu Waziri wa Afrika Mashariki, Mhe. Abdullah J Abdallah, amenusuirika katika ajali ya gari leo jioni katika maeneo ya Tumbi – Kibaha wakati akitokea Bungeni Dodoma akielekea Dar.
Ndani ya gari alikuwa pamoja na mkewe na watoto wake ambao wote wamepata majeraha madogo, dereva wake ameumia zaidi na hivyo kulazimika kukimbizwa katika hospitali ya Tumbi.

Labels: ,

EDWARD LOWASSA: TUPO TAYARI KUINGIA VITANI NA MALAWI NA TUMEJIPANGA VIZURI


KAMATI ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama imesema Tanzania imejiandaa kiakili na kivifaa kuingia vitani na Malawi kama italazimika kufanya hivyo.

Akizungumza mjini Dodoma jana, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Edward Lowassa alisema kamati yake imeridhishwa na maandalizi ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

“Tumepewa maelezo na jeshi letu na tumeridhika kuwa ikibidi kuingia vitani jeshi letu liko vizuri sana na limejipanga vizuri sana kwa uhakika, kiakili na kivifaa,” alisema Lowassa.

Kabla ya Lowassa kuzungumza na waandishi wa habari, alifanya kikao cha faragha kilichohusisha pia wajumbe wa kamati hiyo na makamanda wa JWTZ walipofika bungeni kutoa taarifa kwa kamati hiyo.

 
Hata hivyo, katika tamko hilo Lowassa alisema Tanzania inatarajia mgogoro huo utamalizika kwa njia za kidiplomasia kwa sababu Watanzania na Wamalawi ni ndugu wa muda mrefu.

“Ikibidi kuingia vitani jeshi letu liko vizuri sana na kama ilivyo ahadi yao (JWTZ), wako tayari kulinda mipaka ya nchi yetu hadi tone la mwisho. Tunasali sana tusifike hapo,” alisema Lowassa na kuongeza: “Tunategemea hatutafika huko, lakini kwa heshima ya nchi yetu kama ikibidi kufika huko (vitani) tutafika kulinda mipaka yetu”.

Mwenyekiti huyo ambaye aliwahi kuwa Waziri Mkuu, alisema kama Tanzania itafikishwa mahali itabidi damu ya Watanzania imwagike, nchi iko tayari kulinda mipaka yake kwa nguvu.


Alisema kama itabidi kuingia vitani, itatumia umoja na mshikamano wa Watanzania wa mwaka 1978 wakati wa Vita na Uganda kulinda mipaka ili kulinda heshima ya nchi.

Alisema mwaka 1978 wakati Rais wa Uganda, Idd Amin na majeshi yake walipochukua sehemu ya Tanzania na kujitangazia ni mali yake, ilichukua hatua kumfukuza Amin.

“Alijitangazia sehemu ile ni mali ya Uganda hutegemei nchi ikae kimya, hutegemei Watanzania wanyamaze wakati nchi yao imetekwa, tulichukua hatua tukamfukuza hadi nchini kwake.”

 
Lowassa alisema Kamati ya Bunge inajua madhara ya kiuchumi yaliyotokana na Vita ya Idd Amin na kwamba vita yoyote ikipiganwa lazima kunakuwa na madhara ya kiuchumi.

Hata hivyo, alisema anaamini mgogoro huo hautafika huko na kusisitiza kuwa, lakini ikibidi JWTZ ni moja kati ya majeshi bora duniani na ni jeshi lililojiandaa vizuri kwa lolote.

 
“Wako tayari sisi ni moja kati ya jeshi lililojiandaa vizuri na jeshi bora duniani na la kujivunia. Tuko imara kiakili na kivifaa tena vya kisasa,” alisema Lowassa.

Alisema kamati yake inaunga mkono msimamo ulitolewa bungeni juzi na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe kuhusu mgogoro huo na kwamba ndiyo kauli rasmi ya Serikali.

 
Juzi, Waziri Membe alizionya kampuni za kigeni za Malawi zilizoingia katika ardhi ya Tanzania eneo la Ziwa Nyasa kutafiti mafuta na gesi kusitisha mara moja.

Akiwasilisha makadirio ya wizara yake, Membe alisema upo ushahidi kuwa ndege tano za utafiti za Malawi ziliruka anga la Tanzania na kutua katika Ziwa Nyasa upande wa Tanzania.Membe alisema pamoja JWTZ kutoruhusu ndege hizo za Malawi kuingia na kutua eneo hilo la Ziwa Nyasa, bado ziliingia na kutua kinyume kabisa cha sheria za kimataifa.

“Wenzetu wa Malawi wanadai Ziwa Nyasa lote lipo Malawi na msingi wa madai yao ni mkataba wa Heligoland wa mwaka 1890 na sisi tunasema mpaka uko katikati ya Ziwa.”

Membe alisema hata mgogoro wa mpaka kati ya Cameroon na Nigeria ulitatuliwa na Mahakama Kuu ya Dunia kuwa mpaka baina ya nchi hizo mbili upite katikati ya Ziwa Chad.

Juzi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Malawi, Patrick Kabambe alikaririwa na Redio Sauti ya Ujerumani akisema wataendelea na utafutaji mafuta licha ya onyo hilo la Tanzania.

Waziri huyo alisema ziwa hilo linaitwa Malawi na siyo Ziwa Nyasa na kwamba utafutaji wa mafuta na gesi utaendelea na hakuna wa kuwasimamisha. Alihoji, iweje Tanzania ishtuke sasa

Labels: ,

Tuesday, August 7, 2012

Makutano show ya Fina yageuka gumzo la jiji


Orest Kawau akimkaribisha Fina Mango katika studio za Magic FM kwa ajili ya kuanza kuendesha kipindi chake kipya cha Makutano 

Kipindi cha kwanza cha Makutano kinachoendeshwa na Fina Mango kilianza rasmi jumamosi ya wiki iliyopita. Huu ni ujio mpya wa Fina Mango baada ya kupotea kwenye redio toka wakati akiwa Clouds FM.

Katika kipindi cha Jumamosi Fina alianza kwa kuichambua sheria mpya ya mafao iliyopigiwa kelele na Watanzania wengi ambapo mwanasheria aliichambua na kuielezea ni kwa nini imepingwa na watu wengi kifungu kwa kifungu.
Fina Mango katika picha ya pamoja na Mheshimiwa Zitto Kabwe na Lawrence Masha ambao kabla ya kufanya nao mahojiano kwenye kipindi ambapo walielezea masuala mbalimbali ndani na nje ya siasa.
Mheshimiwa Zitto Kabwe akiongea katika kipindi cha Makutano na kujibu na maswali ya wasikilizaji yaliyotumwa kupitia mitandao jamii
Baada ya hapo Mheshimiwa Zitto Kabwe aliiongea na Fina huku akijibu maswali mengi yaliyotumwa kupitia mitandao ya Twitter, Facebook na Jamii Forums ambayo mengi yalikuwa ya kuhoji kuhusishwa kwake kwenye kashfa ya rushwa, nia yake ya kugombea urais 2015 na uhusiano wake na baadhi ya viongozi ndani ya chama.

Timu ya Makutano Fina Mango, Orest Kawau na Mussa Kipanya katika picha ya pamoja baada ya kipindi.
Mheshimiwa Lawrence Masha akiongea na Fina Mango na kumuelezea mamabo mbalimbali ikiwemo historia yake ya kisiasa.
Wa mwisho kuongea alikuwa Mbunge wa zamani wa Nyamagana na Waziri wa mambo ya ndani Lawrence Masha ambaye alielezea historia yake ya kisiasa na sababu za yeye kushindwa uchaguzi mwaka 2010 kabla hajapewa nafasi ya kuchagua nyimbo 3 anazozipenda na kujibu maswali ya wasikilizaji.

Wengi walionyesha kufurahia ujio mpya wa Fina Mango hasa mjadala uliobaki kwenye mitandao ya kijamii baada ya mahojiano na Zitto Kabwe kumalizika.

Labels: ,

Wednesday, August 1, 2012

MWANAHALISI WAELEZEA SABABU ZA KUFUNGIWA GAZETI LAO..




                                                                         

Siku moja baada ya Serikali kutangaza kulifungia kwa muda usiojulikana gazeti la kila wiki la MWANAHALISI linalochapishwa na kampuni ya Hali Halisi Publishers kutokana na kulituhumu kuandika habari za uchochezi na zinazoleta hofu, Uongozi wa gazeti hilo umezungumza.
Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo Said Kubenea amesema kimsingi hawakupokea barua rasmi kutoka Serikalini inayowataka kusitisha zoezi la kuchapisha gazeti hilo na badala yake hizo taarifa wamezipata kupitia vyombo mbalimbali vya habari.
Kubenea amesema hawakubaliani na madai ya serikali kwamba gazeti hilo limekua likiandika habari za uchochezi na kusisistiza kwamba habari yeyote inayoandikwa katika gazeti hilo ni lazima iwe imefanyiwa uchunguzi wa kina na kamwe gazeti hilo halikuwahi kukurupuka na kuandika habari isiyo ya kweli.
Inaaminika kwamba moja kati ya habari za hatari zilizofanya gazeti hilo kufungiwa kwa muda usiojulikana ni ile ya kuchapisha namba za simu za watu waliowasiliana na Dr Ulimboka mara ya mwisho kabla ya kufanyiwa ukatili.
.
Kwa kusisitiza, Kubenea amesema “hakuna kosa lolote tulilolifanya na tunastahili kupongezwa badala ya kulaumiwa, tulichofanya sisi ni kitu kidogo sana, tuliangalia tu ni nani aliwasiliana na Dr Ulimboka kwa mara ya mwisho… sasa tumepetaje? hizo ni taarifa zetu, kama kuna uchochezi ambao tumeufanya tulipaswa kuwepo Mahakamani lakini mpaka leo hatujaulizwa, hatujahojiwa, hatujaitwa hivyo ina maana hakuna kesi…. mimi kubenea nimefanya uchochezi ni kosa, naweza kufanya kosa kama hilo alafu natembea barabarani? “

Labels:

MAELEZO BINAFSI YA MHE. ZITTO ZUBERI KABWE DHIDI YA TUHUMA ZA RUSHWA HUSUSAN KUELEKEA KATIKA KUPITISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI

                                                                       



MAELEZO BINAFSI YA MHE. ZITTO ZUBERI KABWE DHIDI YA TUHUMA ZA RUSHWA HUSUSAN KUELEKEA KATIKA KUPITISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI

Ndugu Waandishi,
Nalazimika kukutana nanyi kutoa maelezo juu ya tuhuma zenye shinikizo la kisiasa zinazoelekezwa kwangu binafsi kwamba hata mimi nimeshiriki katika vitendo vya rushwa, kwa nafasi yangu kama Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma. Taarifa hizo, kama kawaida ya uzushi mwingine wowote  zimesambazwa kimkakati na kwa kasi kubwa kiasi cha kuukanganya umma.
Nafahamu nabeba dhamana kubwa ya uongozi, taswira yangu ya uongozi daima imeakisi njozi na matumaini ya wananchi wa Kigoma Kaskazini, wananchi wanyonge na vijana kote nchini bila kujali itikadi zao za kisiasa, jinsia zao, makabila yao na rika zao. Hivyo, nawajibika kupitia kwenu kuwatoa hofu juu ya hisia potofu zinazopandikizwa kwao na wale wasiopenda kuona baadhi yetu tukiwaunganisha na kuwasemea watanzania wasio na sauti, dhidi ya vitendo vya hujuma na vyenye dhamira ovu kwa taifa.
Mkakati huo wa kuniunganisha na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaotuhumiwa kwa kupokea Rushwa unatekelezwa kwa njia zifuatazo:
  1.   Kumekuwa na kauli za watendaji wa serikali ambao wamekuwa wakizieneza na hususan kutoa taswira kwamba baadhi ya kauli zangu zinatokana na ushawishi wa rushwa;
  2.   Kuna taarifa ambazo zimeandikwa tena katika kurasa za mbele za baadhi ya vyombo vya habari  zikidai ’’Zitto kitanzini’’ ama ’’Zitto sawa na popo nundu’’  zikiashiria kwamba na mimi ni mla rushwa; na
  3.   Waandishi wa habari na jamii kwa ujumla wamefikia kuaminishwa habari hizi kiasi cha wengine kuuliza kwa nini Mhe. Zitto Kabwe hakutajwa katika orodha iliyotolewa na Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani.
Ndugu Waandishi,
Naomba kutoa ufafanuzi wa hicho kinachoelezwa kwamba nina ushiriki katika masuala ya rushwa hususan kwenye masuala yanayohusu sekta ya Nishati na Madini:-
  1. Mara baada ya bodi ya Wakurugenzi ya  Shirika la Usambazaji wa Umeme Tanzania (TANESCO) chini ya Uenyekiti wake Meja Jenerali Mstaafu Robert Mboma kutangaza kwamba imemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Nd. William Mhando ili kupisha uchunguzi wa baadhi ya vitendo/mwenendo wake, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ambayo mimi ni Mwenyekiti wake ilimuandikia Mhe. Spika kumuomba aridhie ili Kamati iweze kuwaita Bodi ya TANESCO, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali  (CAG) na pia Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kujiridhisha na tuhuma zote zinazotajwa zinafanyiwa uchunguzi wa kina na hatua kuchukuliwa;
  2. Kamati ya POAC ninayoiongoza ilimuomba Mhe. Spika kuwaita wahusika tajwa kwa kuwa zilikuwapo tetesi kuwa kusimamishwa kazi kwa Mkurugenzi huyo siku chache kabla ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kulikuwa na lengo la kufunika ’madudu’ makubwa zaidi kwa kulichagiza Bunge na tukio hilo dogo, mkakati ambao naona umefanikiwa sana. Isitoshe, Kamati kutaka kujiridhisha na hatua za Bodi ni sehemu ya msingi ya utekelezaji wa majukumu ya Kamati yaliyowekwa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge na pia Shirika la TANESCO ni moja kati ya mashirika ambayo yanawajibika kwetu kwa hesabu zake na pia ufanisi wake kwa ujumla. Tumefanya hivyo pia katika mashirika mengine, hili la TANESCO sio tukio la kipekee;
  3. Kitendo hiki cha halali na kwa mujibu wa Kanuni kilichofanywa na Kamati yangu  kimetafsiriwa kwa makusudi na baadhi ya watu kwamba ni ishara ya kuwa sisi au zaidi kwamba mimi nina maslahi binafsi na TANESCO na hususan Mkurugenzi wake Injinia Mhando, ndio maana tumetaka maelezo ya Bodi. Ukweli kwamba Kamati ya POAC tumewaita pia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu (CAG) na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa jambo hilo hilo umefichwa kwa makusudi!
  4. Baada ya  tukio hilo, nikiwa hapa Dodoma, mwandishi wa habari wa gazeti moja alinifuata akiniambia kuwa wamekutana na Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu wake, Nd. Eliachim Maswi hapa hapa Bungeni na wamewaambia kuwa mimi nimepewa rushwa. Hakutaja nimepewa rushwa na nani, kiasi gani na wala kwa lengo gani!
  5. Nimejaribu kumtafuta kwa simu Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu wake ili wanipe ufafanuzi juu ya mimi na Kamati ya POAC kuhusishwa na tuhuma hizi bila mafanikio, hali ambayo inaniondolea mashaka juu ya ushiriki wao katika kueneza au kuthibitisha uvumi huo. Najaribu sana kujizuia kutokuwa na mashaka na ushiriki wao huo ikizingatiwa uzito na taswira ya nafasi zao katika jamii, lakini wameshindwa kunidhihirishia tofauti.
Sasa naomba kutoa ufafanuzi rasmi kuhusu mlolongo wa matukio hayo tajwa ambayo yanatumiwa na baadhi ya wanasiasa kuonesha kwamba eti nimehusika na vitendo vya rushwa.
  1. Binafsi sijawahi kuwa na mawasiliano ya aina yeyote na uongozi wa TANESCO kushawishiwa juu ya hatua ambazo POAC ndio imezichukua za kutaka kujiridhisha juu ya utaratibu uliotumika. Ieleweke wazi kabisa kuwa, hakuna wakati wowote, popote ambapo mimi binafsi au Kamati yetu imekataa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO kuchunguzwa kwa tuhuma zozote. Ambacho tumesisitiza wakati wote ni ufuatwaji wa taratibu, kanuni na sheria, hili nitalisimamia iwe masika au kiangazi;
  1. Ni kwa sababu hiyo, na kwa kujiamini kabisa nimeunga mkono suala la tuhuma za rushwa zinazotajwa zichunguzwe na Kamati ya Haki, Maadili na  Madaraka  ya  Bunge kwa kina;
  1. Nimekwenda mbali zaidi kukiomba chama changu CHADEMA kifanye pia uchunguzi na tathmini yake kwa kina kujiridhisha na tuhuma hizo;
  1. Natumia fursa hii pia kuomba vyombo vya Dola vichunguze tuhuma hizo kwa nafasi yake ili kuweza kupata ukweli;
  1. Ninaahidi kushiriki kikamilifu iwapo nitatakiwa katika uchunguzi wowote utakaofanywa na niko tayari kuwajibika iwapo nitakutwa na hatia yeyote.
Napenda niwatoe hofu wananchi wa jimbo la Kigoma Kaskazini walionituma kuja kuwawakilisha hapa Bungeni na Watanzania wote kwa ujumla kwamba:-
  1. Mimi Zitto Zuberi Kabwe sina bei, sijawahi kuwa nayo na sitarajii kuwa nayo huko mbeleni. Daima nimesimamia kidete maadili ya uongozi bora katika maisha yangu yote ya siasa, na nawaahidi sitarudi nyuma katika mapambano dhidi ya rushwa katika nchi hii pamoja na mikakati ya aina hii ya kunidhoofisha na kunivunja moyo;
  1. Nafarijika na salam mbali mbali zinazotolewa kunifariji na kusisitiza kuwa nisilegeze kamba katika mapambano haya, nimepokea ujumbe mwingi kwa simu, sms, tweeter na hata facebook na niko pamoja nanyi Watanzania wenzangu kamwe sitarudi nyuma hadi kieleweke. Naamini katika nchi yetu tunazo rasilimali za kutosha mahitaji/haja ya kila mmoja wetu lakini si ‘tamaa/ulafi’ wa baadhi ya watanzania wenzetu;
  1. Napenda kuweka rekodi sawa kwa Watanzania kwamba nimekuwa Mbunge hiki ni kipindi cha pili, Mimi ni Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) huu ni takriban mwaka wa saba sasa, Kamati yangu inasimamia mashirika 259 ya Umma na si TANESCO peke yake. Mchango wa Kamati hii katika Bunge na kwa ustawi wa Mashirika ya Umma ni bayana na haujawahi kutiliwa shaka. Kamati yetu imeokoa upotevu mkubwa wa mali za umma na kuokoa fedha za umma kutokana na umakini wake. Tumefanya hivyo CHC hivi karibuni, Kiwira na kwenye mashirika mengine mengi. Kote huko uadilifu na uzalendo wa Kamati hii haujawahi kuhojiwa. Inatuwia vigumu kuona kuwa tunahojiwa katika suala hili la TANESCO. Hapa pana kitendawili.
  1. Zipo hoja pandikizi za kutaka Kamati ya POAC ivunjwe na haswa zikinilenga mimi binafsi. Nafahamu kiu ya wasioitakia mema nchi yetu kuiona POAC ikivunjwa au sura zikibadilishwa kwa kuwa Kamati hii imekuwa mwiba kwa mikakati yao ya kifisadi. Kwa maoni yangu, Kamati ya POAC isihusishwe na tuhuma hizi kwa vyovyote vile. Niko tayari nihukumiwe mimi kama mimi na sio kuhusisha wajumbe wengine ambao hawatajwi mahala popote katika tuhuma hizi mbaya sana katika historia ya Bunge letu. Nitakuwa tayari kunusuru Kamati ya POAC na maslahi ya taifa letu kwa kujiuzulu Uenyekiti iwapo itathibitika pasipo shaka kuwa nimehongwa. Kamati ya POAC ni muhimu zaidi kuliko mimi.
  1. Nafahamu pia kuwa kuna wanasiasa hasa wa Upinzani ambao wanautaka sana Uenyekiti wa POAC na wanafanya kila njia kutaka kuidhoofisha. Lakini hawajui kuwa anaepanga wajumbe wa Kamati ni Spika wa Bunge.
  1. Msishangae pia kuja baadae kubaini kwamba baadhi ya wanasiasa wenye midomo mikubwa ya kutuhumu wenzao wao ndio vinara wa kupokea rushwa.
  1. Ni lazima tufike mahali kama viongozi kwamba utaratibu unapokiukwa na yeyote yule, au uongo unapotolewa hadharani tuseme bila kuogopa. Hili ndio jukumu letu kama wabunge na viongozi. Kusimamia ufuatiliaji wa utaratibu ni jukumu letu kama Kamati ya POAC na ndio sababu ya msingi ya kuanzishwa kwa mamlaka kama CAG na PPRA. Haiwezekani, tuwe na set ya kanuni kwa kundi fulani na nyingine kwa makundi mengine, au kuhukumu ufuataji wa taratibu kwa kuangalia sura ya mtu usoni
Mwisho
Kumejengeka tabia hivi sasa ya kuwamaliza wanasiasa wenye kudai uwajibikaji na uzalendo. Kumeanzishwa kiwanda kwenye medani ya siasa cha kuzalisha majungu na fitna zenye lengo la kuwachonganisha wanasiasa wa aina hiyo na wananchi kwa kutumia vyombo vya habari na nguvu ya fedha. Naamini mbinu hizi chafu, kama nyingine nyingi zilizojaribiwa kwangu huko nyuma nazo zitashindwa.
Naamini katika kweli na kweli daima huniweka huru. Naamini kuwa mwale mdogo wa mwanga wa mshumaa hufukuza kiza. Kwa imani hiyo, sitasalimu amri mbele ya dhamira zao ovu hata nitakapobaki peke yangu katika mapambano hayo ya kulinda na kutetea rasilimali za taifa zinufaishe watanzania wote.
Daima nitaongozwa na busara ya Hayati Shabaan Robert isemayo, ‘Msema kweli huchukiwa na marafiki zake, nitakapofikwa na ajali hiyo, sitaona wivu juu ya wale wawezao kudumu na marafiki zao siku zote, siwezi kuikana kweli kwa kuchelea upweke wa kitambo, nikajitenga na furaha ya kweli itakayotokea pale uwongo utakapojitenga”.
Ahsanteni sana.

Labels:

Monday, July 30, 2012

ZITTO KABWE ATOA KAULI KALI SANA LEO..

Labels:

Tuesday, July 24, 2012

MBUNGE (MDEE) ALIYEMTOA MACHOZI ZITTO ANG'AKA... ZITTO AJIBU URAISI 2015..

Mdee Naye amkana Zitto
Kwenye barua yake kwenda kwa uongozi wa juu wa gazeti la mwananchi, hii ni sehemu ya barua yake.

Nasikitika kutumia nafasi hii kukuandikia kukutaarifu kuwa gazeti lako la Mwananchi la Julai 23, 2012, katika habari yake iliyoongoza ukurasa wa kwanza (lead story) limenilisha maneno na kunikuu isivyo sahihi.

Katika habari hiyo yenye kichwa cha habari kisemacho “Wabunge wamsafishia Zitto njia ya urais 2015,” gazeti lako limeandika hivi “Mdee aliyepewa nafasi ya kuwasalimia wananchi alisema amekuwa na Zitto tangu Chuo kikuu cha Dar es Salaam na kwamba kutokana na ujasiri na umahiri wake katika kutetea masilahi ya wanyonge na taifa, anafaa kuwa mmoja wa viongozi wa juu katika Taifa.”



Gazeti lako pia katika aya iliyofuata limenukuu kuwa mimi nimesema;

*“Ndugu zangu watu wa Kigoma, kwa kweli mna bahati sana, achilia mbali kuwa na vipaji katika sanaa ya muziki na michezo hasa mpira wa miguu, lakini mna wanasiasa wakali ambao ni tishio hapa nchini. Mimi namkubali sana Zitto Kabwe na ninaamini kuna siku atakuwa kiongozi wa juu katika nchi yetu," alisema Mdee”



Nasikitika kusema kuwa gazeti lako limeandika habari zisizo za kweli kwa kunilisha *maneno na kudai kuwa mimi ndiye nimesema maneno hayo, kisha kuyaweka kwenye nukuu, likisema kuwa ni nukuu yangu. Sijajua nia au kusudio la gazeti lako kuamua kupotosha ukweli na kushindwa kabisa kuninukuu kwa usahihi, kama inavyotakiwa katika misingi ya taaluma ya habari.

Nasikitika pia kusema kuwa gazeti lako ambalo limeonekana kujijengea heshima miongoni mwa wasomaji wa kada mbalimbali nchini na hivyo linapaswa kuwa mfano wa kuigwa, linaweza kusigina misingi ya uandishi wa habari na hususan katika kufuata maadili ya taaluma hii muhimu, kwa kiwango cha kufanya moja ya dhambi kubwa ya kukilisha maneno chanzo cha habari.

Kwa ajili ya kutunza heshima ya gazeti lako, lakini pia kwa ajili ya maslahi mapana ya taaluma ya habari na jamii ya Watanzania, nakuandikia kulitaka gazeti lako likanushe maneno liliyoninukuu katika toleo hilo la Julai 23, 2012. Ni vyema sana hilo likafanyika kwa uzito unaostahili kama ilivyoandikwa katika toleo hilo.



Habari hiyo imeniletea usumbufu mkubwa hasa kwa wanachama wa chama changu, CHADEMA, ambao wanajua kuwa chama chao makini ni mahiri katika kufuata katiba, kanuni na taratibu katika kuendesha mambo yake kwa manufaa ya watu wote. Napenda kuwa mmoja wa Watanzania makini na viongozi wanaojua wajibu, ikiwemo kufanya nini na kusema nini, mahali gani na wakati gani.



Nakutakia utekelezaji mwema katika hilo

ZITO ZUBERI KABWE ANASEMA..
Katika gazeti la Mwananchi la tarehe 23 Julai 2012, kulikuwa na habari yenye kusomeka 'Wabunge wamsafishia Zitto njia ya Urais 2015'. Habari hii imeleta mjadala mara baada ya kutoka na kusomwa. Mjadala umekuzwa zaidi baada ya Wabunge ndugu Halima Mdee na ndugu Joshua Nassari kukanusha maneno waliyonukuliwa kusema. Napenda kusema masuala yafuatayo.

Moja, Waheshimiwa Wabunge Halima Mdee, Joshua Nassari, Kangi Lugola, Esther Bulaya, Deo Filikunjombe, Raya Ibrahim, Amina Mwidau na David Kafulila walihudhuria tamasha la vijana wa Kigoma All Stars kwa kualikwa na Mratibu wa kundi hilo Mwasiti Almasi.

Wabunge wengine walialikwa lakini hawakutokea wakiwemo Joseph Mbilinyi, David Silinde, Amos Makala, Vicky Kamata na Peter Serukamba. Wabunge hawa hawakualikwa na mimi na wala sikufanya mazungumzo nao yeyote ya awali au kuwaambia au kukubaliana nini cha kuzungumza au hapana. Tamasha lilikuwa la muziki na halikuhusika kabisa na siasa.

Waheshimiwa wote walipewa nafasi ya kusalimia na wote walizungumza. Wabunge waliozungumza kwa muda mrefu kidogo ni ndugu Halima Mdee, Joshua Nassari, Deo Filikunjombe na Kangi Lugola.

Hotuba za Wabunge wote zilirekodiwa kwenye video neno kwa neno na video hizo zitawekwa wazi kwenye blogu yangu kama sehemu ya documentary ya tamasha lile la kihistoria.

Pili, sikuhusika kwa namna yeyote ile na kuandikwa kwa habari hii iliyozusha mjadala. Wala sikujua kama habari hii ingeandikwa maana katika ziara ile sikuita mwandishi hata mmoja maana nilitaka liwe tukio la Kigoma tu.

Kama mwandishi kaandika ambayo wabunge hawa hawakuyasema basi itaonekana kwenye videos hizo. Wabunge wenyewe wanajua kwenye nafsi zao nini walisema Kigoma na kipi kiliwasukuma kusema walioyasema Kigoma. Nisingependa kuhusishwa kwa njia yeyote ile na matamshi yao, habari iliyowanukuu na hata makanusho yao. Maana mwisho wa siku ukweli ndio utasimama.

Suala la Urais lisitupotezee muda kwani kuna mambo mengi sana ya kujadili kuhusu nchi yetu. Taharuki ambazo watu wanazipata masuala ya urais yanapotajwa zinashangaza sana.

Chama changu bado hakijatangaza rasmi mchakato wa kupata mgombea Urais. Hivi sasa chama hakina mgombea Urais mpaka hapo mchakato utakapotangazwa ambapo wanachama wataruhusiwa kuomba kupeperusha bendera ya chama. Mwanachama wa chama chetu atakaye kubalika na jamii na wajumbe wa mkutano wa uteuzi ndiye atakuwa mgombea wetu. Kwa sasa hayupo na hivyo tusipoteze muda kujadili jambo hili.

Mzee Thabiti Kombo alituachia usia tunapokuwa tunazungumza. Alisema 'weka akiba' sio akiba ya fedha, bali ya akiba ya maneno. Tuweke akiba ya maneno. Tusimalize yote.


Source; Jamii Forum 

Labels: ,